Home » » M23 WASALITI AMURI

M23 WASALITI AMURI

Written By kitulofm on Wednesday, 6 November 2013 | Wednesday, November 06, 2013

Vikosi vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) vilivyopo kwenye vikosi vya Umoja wa Mataifa, vimeongeza kasi ya kukabiliana na waasi wa Kundi la M23 na kufanikiwa kutwaa maeneo mengine zaidi ikiwemo Milima ya Mbuzi iliyokuwa ikitumika kama maficho kwa waasi hao.

Eneo la Milima ya Mbuzi lililoko karibu na mpaka na Uganda ni moja ya ngome za mwisho za kundi hilo ambalo lilianza kupoteza udhibiti wa maeneo muhimu tangu mwishoni mwa mwezi uliopita wakati vikosi vya Congo kwa msaada wa vile vya Umoja wa Mataifa vilipoanzisha operesheni maalumu ya msituni.
Kuzuka kwa mapigano hayo kumekuja wakati kukiwa na taarifa zinazokinzana kutoka pande zote mbili kuhusiana na usalama wa eneo hilo la Mashariki.
Wakati Vikosi vya Congo vikiwa vimetangaza operesheni mpya iliyopewa jina la “Mkakati wa kufagia masalia ya waasi”, naye kiongozi wa M23, Bertrand Bisimwa aliwataka askari wake kuweka chini silaha ili kurejea kwenye meza ya mazungumzo nchini Uganda.
Duru za habari zinasema kuwa askari wa Congo wakishirikiana na wale wa Umoja wa Mataifa wameendesha mashambulizi ya angani na kufanikiwa kuwafurusha wanamgambo wa M23 walioweka kambi maeneo ya Runyonyi na Chanzu umbali wa kilometa 80 Kaskazini mwa Mji wa Goma. Imesemekana pia katika mapigano hayo raia sita walipoteza maisha.
Msemaji wa vikosi vya Umoja wa Mataifa Martin Kobler alisema jana kuwa kitendo cha waasi wa M23 kuanzisha mashambulizi kwa raia wakati walitangaza kuweka chini silaha ili kupisha mazungumzo ya amani ni kitendo kisichokubalika.
Alisema kuwa mwenendo ulionyeshwa na M23 kutosimamia kauli zake, ndiyo sababu vikosi vya Umoja wa Mataifa kuendesha mashambulizi ya angani na kuhaidi kufanya hivyo mpaka pale waasi hao watapofurushwa kabisa katika ardhi ya Congo.
Hata hivyo kumekuwa na utata kuhusiana kuuawa kwa raia sita ambao miili yao ilikutwa jana kwenye eneo la Bunagana lililoko mpakani na Uganda.
Akizungumza na shirika la habari la AFP, Gavana wa jimbo la Kivu Kaskanizi Julien Paluku hakuwa tayari kutaja upande uliosababisha mauaji hayo.
Afisa wa Jeshi la Uganda, Luteni Kanali Paddy Ankunda alisema mapigano hayo yalisababisha pia uharibifu katika maeneo ya Uganda lakini hakuna raia yoyote aliyejeruhiwa.
Hivyo baadhi ya ripoti zinasema tangu kuanzishwa kwa operesheni ya awamu ya pili zaidi ya raia tano wa Uganda wamejeruhiwa. Kumekuwa na taarifa kuwepo kwa hali ya shamra shamra kutoka kwa askari wa Congo walioingia katika Milima ya Mbuzi.
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

KITULO FM LOGO

KITULO FM LOGO
Tusikilize masaa 18 kwa siku kupitia masafa ya 97.0 FM ukiwa wilayani Makete mkoani Njombe na maeneo ya jirani

WASOMAJI WETU

KUMBUKUMBU YA HABARI ZETU

 

Copyright © 2013. KITULOFM BLOG - Haki zote zimehifadhiwa
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inawezeshwa na Kitulo Fm