Na Shariff Mbukuzi, Zanzibar
VIONGOZI wa nafasi za kisiasa Zanzibar wamethibitika kujiingiza katika fedheha kubwa kutokana na ulafi wa kumiliki ardhi.
Uchunguzi wa migogoro mbalimbali ya ardhi uliofanywa na kamati teule
ya Baraza la Wawakilishi umebaini kuwa viongozi waandamizi serikalini na
katika Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamepewa maeneo kimabavu. Kwa mujibu
wa ripoti ya kamati hiyo iliyoongozwa na Mwakilishi wa Kuteuliwa, Ali
Mzee Ali, ugawaji wa ardhi kwa viongozi kadhaa ulifanywa kinyume cha
sheria za ardhi za Zanzibar.
“Waliotajwa ambao tulipowaita wafike mbele ya kamati yetu
walishindwa kutoa vielelezo vya namna walivyomilikishwa maeneo ya
ardhi, ni pamoja na viongozi na baadhi ya watoto wa viongozi,” Baraza
liliambiwa na Mzee alipokuwa akiwasilisha ripoti hiyo, wiki iliyopita.
Baraza liliazimia kuundwa kamati ya uchunguzi ili kuchunguza
malalamiko ya wananchi yaliyolifikia baraza hilo kupitia kwa wajumbe
wake, baada ya kuwepo tuhuma za kufutwa kwa hatimiliki za baadhi ya
maeneo pasina kufuatwa sheria zilizopo.
Baadhi ya maeneo yaliyolalamikiwa – yakiwemo kwenye maeneo ya karibu
na fukwe za Bahari ya Hindi – yalikuwa yakitumiwa na wananchi kwa
kuchimba mchanga wa kujengea, na mengine kwa shughuli za kilimo.
Hadidu rejea zilizopangwa kufanyiwa kazi katika uchunguzi wa kamati
teule ya Baraza, ni kuangalia mgogoro wa ardhi baina ya serikali,
wananchi na wakulima wa kijiji cha Bambi, Wilaya ya Kati; mgogoro wa
mfanyabiashara na wakulima wa kijiji cha Tumbe, Wilaya ya Micheweni;
mgogoro wa wananchi na serikali iliyoyatoa maeneo kwa ajili ya uwekezaji
wa vitega uchumi kijiji cha Makangale, Wilaya ya Micheweni na mgogoro
baina ya wananchi na viongozi wa serikali eneo la Mchangamle, Kizimbani,
Wilaya ya Wete.
Migogoro mingine ya ardhi iliyochunguzwa ni uliohusu wananchi wa
Vitongoji Makaani, Wilaya ya Chake Chake; ule uliohusu mwekezaji na
wananchi kijiji cha Pwanimchangani, Wilaya ya Kaskazini B; mwingine
uliohusu wananchi na viongozi wa ngazi ya juu serikalini eneo la
Tondooni Mkunguni, Pemba.
Mgogoro baina ya Idara ya Upimaji na Ramani na Wizara ya Kilimo eneo
la Tumbe, Wilaya ya Micheweni ambao umetoa mwanya kwa wananchi kuvamia
eneo hilo kwa shughuli za kilimo; mgogoro baina ya mwekezaji na wananchi
eneo la Mzwardini, kijiji cha Bwejuu, Wilaya ya Kusini, Unguja.
Uchunguzi umebaini kwamba sheria za ardhi zimekiukwa na watendaji wa
serikali kutajwa kama waliotoa mchango mkubwa katika uvunjaji wa sheria
za ardhi.
Kamati ya uchunguzi ya Baraza la Wawakilishi ilibaini kuwa baadhi ya
hatimiliki zilifutwa bila ya taratibu za kisheria, ikiwemo kumuarifu
mmiliki wa awali kuhusu nia ya serikali kutwaa eneo.
Kwa mfano, uchunguzi umebaini, katika eneo linalogombaniwa na
mwananchi aitwaye Ali Muradi na kampuni ya Zanzibar Dairy Products,
mwekezaji alimilikishwa eneo hilo bila ya hati ya mwananchi kufutwa.
Katika mgogoro huo, kamati imesema, mawaziri wawili walioshika
wadhifa wa wizara ya ardhi, walitoa hati ya kufuta kwa muda umiliki wa
eneo kwa mmiliki wa awali, mwananchi, na kutoa hati mpya kwa mwekezaji
huyo.
Kamati imesema si jambo la kawaida serikali kuidhinisha mmiliki
aliyefutiwa hatimiliki ya eneo moja, kupatiwa eneo jingine kama
ilivyotokea kwa mgogoro huo. Muradi alipewa eneo jingine na wizara
ingawa sababu ya kufutiwa milki eneo la awali, ilielezwa kuwa ni
kushindwa kuliendeleza.
“Utaratibu huo si wa kawaida kwa anayefutiwa hati kupatiwa eneo
jengine, huku wizara hiyo katika taarifa yake kwa Kamati ilieleza kuwa
eneo hilo lilifutwa kutokana na kuwahi kupewa mtu mwengine na hivyo
kuamua kufuta hati ya Muradi kwa msingi huo. “Kamati baada ya kuitaka
Wizara kuwasilisha kwao hati ya matumizi ya ardhi iliyotolewa awali,
ilishindwa licha ya kuandikiwa barua mara kadhaa hadi wakati kamati
ikikamilisha kazi yake,” alisema mwakilishi Mzee.
Akizungumzia mgogoro wa mfanyabiashara na wakulima wa kijiji cha
Tumbe, Wilaya ya Micheweni, mwenyekiti wa kamati hiyo ya uchunguzi ya
Baraza la Wawakilishi alisema mwaka 2010 kamati ya kudumu ya baraza
(Kamati ya Mawasiliano) ilitembelea eneo hilo na kuagiza asilimia 70 ya
eneo hilo wapatiwe wananchi ambao wamekuwa wakitumia eneo hilo kwa
kilimo.
Hata hivyo, alisema serikali kupitia wizara ya ardhi, haikuzingatia
agizo hilo. Matokeo yake, kamati ilikuta, eneo kubwa waligawiwa viongozi
wa juu serikalini, na kuwataja mawaziri, spika wa baraza, wakuu wa
mikoa na wilaya pamoja na wakuu wa kamati za ulinzi na usalama wa maeneo
hayo.
Ripoti ya kamati imetaja kwa majina viongozi waliopewa ardhi eneo la
Tumbe kuwa ni Shamsi Vuai Nahodha (Mwakilishi wa Mwanakwerekwe na
Mbunge wa Kuteuliwa), Mbunge wa Uzini, Muhammed Seif Khatib na Mbunge
wa Makunduchi, Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi
ya Makamu wa Rais anayesimamia Muungano.
Majina mengine yaliyotajwa katika ripoti hiyo ni wanasiasa wakongwe
wa jimbo la Donge, Ali Ameir Mohamed na Ali Juma Shamhuna (waziri katika
Serikali ya Umoja wa Kitaifa, Zanzibar), Suleiman Othman Nyanga
(Mwakilishi wa Jang’ombe na waziri), Asha Abdalla Juma, aliyekuwa waziri
serikali, Amani Karume sasa akiwa mjumbe wa Sekretarieti ya CCM na Dk.
Maua Daftari, mbunge Viti Maalum (CCM) mwenyeji wa Wete, Pemba.
Katika mgogoro wa ardhi baina ya wawekezaji eneo la Matemwe, Wilaya
ya Kaskazini A, kamati ilibaini kuwa mwekezaji kampuni ya Al Nakheel,
aliyekodishwa eneo awali kujenga hoteli, alifutiwa hatimiliki kwa madai
ya kushindwa kuliendeleza.
Kamati iliona katika uchunguzi wake kuwa kulikuwa na barua
ilizoandikiwa kampuni ya Leisure Corp kujulishwa kufutiwa hatimiliki
siku moja na kuhalalishwa kwa eneo hilo kwa kampuni nyingine tatu
kutumia eneo husika.
Maofisa wa wizara waliiambia kamati kwamba hatimiliki za kampuni
tatu baadaye, zilifutwa kwa sababu miradi yao haikuidhinishwa kisheria
kutokana na kutopitishwa na Mamlaka ya Uwekezaji Vitegauchumi Zanzibar
(ZIPA). ZIPA imeanzishwa kwa Sheria ya mwaka 1992, na uidhinishaji wa
miradi ya vitegauchumi hufanywa kupitia Kifungu 46(3) kinachohusu
matumizi ya ardhi kwa shughuli za uwekezaji vitegauchumi.
Kamati katika hatua nyingine ikielezea uamuzi wa serikali kufuta hati
ya ukodishaji wa ardhi eneo la Uroa kwa mwekezaji Bruno Konti kwa muda
wa miaka 33, ilisema imebaini kuwa badala yake eneo hilo walilojenga
hoteli, alimilikishwa mtoto wa waziri katika serikali aliyoongoza Amani
Abeid Karume.
Hata hivyo, hakuna kielelezo hata kimoja wala maelezo ya mdomo
yaliyotolewa na maofisa wa wizara kuthibitisha uamuzi huo kwa maandishi
kama sheria inavyotaka.
Mwakilishi Mzee alisema katika kuwasilisha ripoti ya uchunguzi kuwa
kamati yake ilibaini ukiukaji mkubwa wa taratibu za kukodisha visiwa
vidogo vya kitalii nje ya bandari ya Malindi, Zanzibar.
Baadhi ya waliokodishwa walitozwa kiwango kidogo cha fedha za kukodi,
kuliko waombaji wengine waliokuwa tayari kulipa fedha nyingizaidi.
Miongoni mwa mapendekezo ya Kamati ya Mzee ni serikali kurudisha
umilikaji wa maeneo kwenye himaya yake na kutangaza ukodishaji ili
wanaotaka kuwekeza waombe rasmi.
Chanzo: Fahamu
0 comments:
Post a Comment