Home » » RAIS KIKWETE"NI UKOSEFU WA ADABU KUWATUKANA WAASISI WA TANZANIA

RAIS KIKWETE"NI UKOSEFU WA ADABU KUWATUKANA WAASISI WA TANZANIA

Written By kitulofm on Friday 18 April 2014 | Friday, April 18, 2014

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa ni utovu wa nidhamu na ukosefu wa adabu kuwa baadhi ya Watanzania kuwatukana, kuwadhihaki na kuwakejeli Waanzilishi wa Taifa la Tanzania, Hayati Julius Nyerere na Hayati Sheikh Abeid Amaan Karume.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa viongozi hao wawili wameifanyia Tanzania mambo mengi, mambo makubwa na mambo ya kihistoria kiasi cha kwamba Watanzania wanao wajibu wa kudumisha na kuenzi heshima yao kwa namna ya kudumu.
Akizungumza na Wahariri wa baadhi ya vyombo vya habari usiku wa jana, Jumatano, Aprili 16 katika mahojiano maalum ya kuadhimisha Miaka 50 ya Muungano, Rais Kikwete amesema: “Ni kukosa adabu na ni utovu mkubwa wa nidhamu kwa Mtanzania yoyote kuwatukana, kuwadhihaki ama kuwakejeli waasisi wa Taifa letu. Hawa ni watu ambao waliifanyia nchi yetu mambo makubwa,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Mzee Karume yule aliongoza Mapinduzi yaliyoondoa dhuluma na uonevu pale Visiwani. Waafrika walio wengi walikuwa wanaonewa sana pale Tanzania Visiwani, pengine watu wamesahau, lakini hata pale walipokuwa wanashinda uchaguzi bado walikuwa hawapewi nafasi ya kuongoza maisha yao wenyewe.”
Amesisitiza Rais Kikwete: “Ni ukosefu wa adabu kwa yoyote kumshutumu mtu aliyejitolea kiasi hicho ili kubadilisha mfumo dhalimu na kujenga maisha na mazingira ya maisha bora kwa wengi.”
“Mzee Nyerere yule ametuachia Taifa moja, lililoungana, lenye umoja, lenye amani na mshikamano. Misingi ambayo aliijenga yeye ndiyo imeendelea kuongoza Taifa letu kwa miaka yote hii. Viongozi wengine wote ambao wamemfuata yeye – Mzee Mwinyi, Mzee Mkapa na sasa mimi mwenyewe, tumefuata na kuongozwa na misingi hii. Na siku nchi yetu inaamua kuipuuza misingi hiyo, tutaingia katika matatizo makubwa.”
Rais Kikwete ametoa msimamo huo baada ya kuwa ameulizwa kuhusu matusi, kejeli, dhihaki ambazo zimekuwa zinaonyeshwa na wajumbe wachache wa Bunge Maalum la Katiba juu ya waasisi hao wa Tanzania na Wabunifu Wakuu wa Muungano wa Tanzania.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
17 Aprili, 2014
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

KITULO FM LOGO

KITULO FM LOGO
Tusikilize masaa 18 kwa siku kupitia masafa ya 97.0 FM ukiwa wilayani Makete mkoani Njombe na maeneo ya jirani

WASOMAJI WETU

KUMBUKUMBU YA HABARI ZETU

 

Copyright © 2013. KITULOFM BLOG - Haki zote zimehifadhiwa
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inawezeshwa na Kitulo Fm