Home » » MWALIMU ATUPWA JELA MIEZI 6 KWA KUTELEKEZA FAMILIA NA KWENDA KUISHI NA KIMADA

MWALIMU ATUPWA JELA MIEZI 6 KWA KUTELEKEZA FAMILIA NA KWENDA KUISHI NA KIMADA

Written By kitulofm on Tuesday 15 April 2014 | Tuesday, April 15, 2014

Mwalimu wa Shule ya Msingi Misunkumilo, Kata ya Namanyere, wilayani Nkasi, mkoani Rukwa, Oswald Kapota (33) amehukumiwa kwenda jela miezi sita kwa kosa la kutelekeza familia yake na kwenda kuishi kwa kimada.

Mwalimu huyo ambaye ameshindwa kubaki njia kuu na kuendeleza michepuko, amepata hukumu hiyo juzi baada ya Mahakama ya Mwanzo Namanyere, kumtia hatiani.

Akitoa hukumu hiyo, Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Namanyere, Baraka Stanley, alisema kuwa mahakama hiyo imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka ambao unaonyesha kuwa Mwalimu huyo alifanya kitendo hicho kwa kukusudia.

Mwalimu huyo alidaiwa kuitelekeza familia yake ya watoto wawili na mke, kisha kuhamia nyumbani kwa  mwanamke mwingine na kuifanya familia hiyo kuishi katika mazingira magumu kwa kipindi cha zaidi ya miezi sita, hali iliyomlazimu mkewe kufungua kesi polisi ya kudai huduma ya malezi ya familia hiyo.

 Licha ya hukumu hiyo mahakama imeamuru mwalimu huyo atakapomaliza adhabu yake ya kifungo jela atalazimika kuitunza familia yake kama wajibu unavyomtaka kama mzazi.

Awali upande wa mashitaka uliieleza mahakama hiyo kuwa mwalimu huyo alimtelekeza  mke wake, Lucy Malambugi, ambaye amezaa naye watoto wawili kiasi cha kuifanya iishi maisha magumu huku mkewe akihangaika kuomba omba ilhali yeye akiponda raha na nyumba ndogo.

Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, mshitakiwa alitakiwa kujitetea ambapo alikataa kutoa utetezi wake kwa madai kuwa hawezi kujitetea mbele ya mwanamke huyo, akimtuhumu kuwa  si mwaminifu kwenye ndoa na ndiyo chanzo cha yeye kuamua kuhamia kwa nyumba ndogo.

Kutokana na kosa hilo, mahakama imemtia hatiani mtuhumiwa huyo chini ya kifungu cha sheria namba 167, sura ya 16, ambayo imefanyiwa marekebisho mwaka 2002.

CHANZO:Tanzania Daima
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

KITULO FM LOGO

KITULO FM LOGO
Tusikilize masaa 18 kwa siku kupitia masafa ya 97.0 FM ukiwa wilayani Makete mkoani Njombe na maeneo ya jirani

WASOMAJI WETU

KUMBUKUMBU YA HABARI ZETU

 

Copyright © 2013. KITULOFM BLOG - Haki zote zimehifadhiwa
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inawezeshwa na Kitulo Fm