Home » » ZANZIBAR WAWEKWA KITIMOTO

ZANZIBAR WAWEKWA KITIMOTO

Written By kitulofm on Friday, 21 March 2014 | Friday, March 21, 2014

Kificho jana alikana maoni hayo ya kutaka serikali tatu na kwamba kilichoelezwa na Jaji Warioba siyo tafsiri sahihi ya mapendekezo yao
Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) juzi jioni walipata wakati mgumu katika kikao cha ndani cha wabunge wa chama hicho wakituhumiwa kwa ‘usaliti wa Muungano’.
Kilichowaponza wajumbe hao ni kupitisha mabadiliko ya Katiba mwaka 2010 yanayoitaja Zanzibar kuwa ni nchi na hivyo kuvunja Katiba ya Muungano na kitendo cha baraza hilo kupendekeza Serikali tatu mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Kikao hicho kilifanyika muda mfupi baada ya Jaji Joseph Warioba kuwasilisha Rasimu ya Katiba akieleza kuwa changamoto kubwa za Serikali mbili ni uvunjaji wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano, uliotokana na Mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.
Katika hotuba yake, Jaji Warioba alisema pia kuwa baraza hilo lilipendekeza mfumo wa Serikali tatu kutokana na maelezo kuwa linataka Zanzibar huru, Tanganyika huru na Serikali ya Muungano huru na kila chombo kuwa na mamlaka yanayotambuliwa.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho kilichoongozwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, zinaeleza kuwa wabunge wa CCM hasa wa Bara walielekeza lawama kwa viongozi wa Zanzibar hasa Baraza la Wawakilishi kutokana na kuwasaliti.
Chanzo chetu kimemtaja mmoja wa wazungumzaji, Christopher Ole Sendeka kwamba alieleza kwa uchungu kuwa mabadiliko yaliyofanywa na Zanzibar ni usaliti mkubwa kwa Serikali ya Muungano.
“Sendeka aliongea kwa uchungu kuhusu Zanzibar kuvunja Katiba ya Muungano na alisema lazima chama kichukue hatua ili kunusuru Muungano,” alisema mjumbe mmoja wa kikao hicho.
Alipoulizwa kuhusu kauli hizo, Sendeka hakukanusha wala kukubali, bali alisema hayo ni masuala ya kikao cha ndani na hawezi kuyazungumzia.
Mbunge mwingine aliyetajwa kuzungumza ni Silivester Mabumba wa Jimbo la Dole, ambaye alieleza wazi kuwa ni vyema kuacha unafiki kuwa mnataka Serikali mbili wakati kuna mabadiliko ambayo mmepitisha kuwa Zanzibar ni nchi. Hata hivyo, Spika wa Bunge la Baraza la Wawakilishi, Pandu Amir Kificho baada ya kushambuliwa alieleza kutofautiana na kile ambacho kimeelezwa katika hotuba ya Jaji Warioba.
Kificho, licha ya kukiri kuwa mmoja wa waliosaini taarifa ya baraza hilo, alisema bado msimamo wa baraza ulikuwa ni Serikali mbili. Kauli hiyo ilithibitishwa jana baada ya kufafanua katika kituo kimoja cha televisheni kuwa msimamo wa baraza haujawahi kuwa ni Serikali tatu.
Baada ya lawama nyingi, inadaiwa wajumbe hao, walifikia azimio la kuandaa utaratibu wa kufanyia mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar kupitia kura ya maoni.
“Tumewaambia waone uwezekano wa kuifanyia marekebisho Katiba yao kama ukipitishwa muundo wa Serikali mbili,” alisema mjumbe mmoja.

CHANZO:MWANANCHI
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

KITULO FM LOGO

KITULO FM LOGO
Tusikilize masaa 18 kwa siku kupitia masafa ya 97.0 FM ukiwa wilayani Makete mkoani Njombe na maeneo ya jirani

WASOMAJI WETU

KUMBUKUMBU YA HABARI ZETU

 

Copyright © 2013. KITULOFM BLOG - Haki zote zimehifadhiwa
Imetengenezwa na Edwin Moshi
Inawezeshwa na Kitulo Fm